SUAMEDIA

Watafiti wa SUA na Denmark wamekutana kujengeana uwezo wa namna ya kutumia matokeo ya kisayansi

 

Na: Farida Mkongwe

Watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA na Watafiti kutoka nchini Denmark wamekutana katika warsha ya mafunzo ya siku mbili kwa lengo la kujengeana uwezo wa namna ya kutumia matokeo ya kisayansi katika kushawishi jamii pamoja na watunga sera katika kufanya mabadiliko yatakayoleta maendeleo ya wananchi.

Mkurugenzi, Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalam Prof. Esron Karimuribo akizungumza baada ya kufungua Warsha ya mafunzo ya siku mbili kwa lengo la kujengeana uwezo wa namna ya kutumia matokeo ya kisayansi kwa kushirikiana na Watafiti kutoka nchini Denmark, leo SUA. 


Akifungua Warsha hiyo mjini Morogoro Machi 16, 2022 Mkurugenzi, Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalam kutoka SUA Prof. Esron Karimuribo amesema mara nyingi watafiti wamekuwa wakifanya tafiti nyingi lakini kumekuwa na changamoto ya namna ya kuwasilisha tafiti hizo kwa wananchi na watunga sera.

“Ni tukio ambalo kwetu tunaliona ni muhimu sana, mara nyingi watafiti wetu wamekuwa wakifanya tafiti tu katika maeneo tofauti ambayo yamelenga kuboresha maisha ya wananchi, lakini jinsi gani ambayo wanawasilisha kwa walengwa inakuwa ni changamoto, kwa hiyo warsha hii inalenga kujenga uwezo wa watafiti katika kutoa ushauri mzuri kulingana na matokeo ya utafiti”, amesema Prof. Karimuribo

Prof. Karimuribo amesema baada ya warsha hiyo ya siku 2 kumalizika watakutana na wadau wengine kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Kilimo, pamoja na Taasisi za Kitaifa za Kitafiti ili kujadili jinsi ya kutumia uwezo wa watafiti kisayansi katika kuboresha maisha ya wananchi wakiwemo wakulima na wafugaji.

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa Kujenga Uwezo kwa Vyuo Vikuu BSU  Prof. Antony Sangeda amesema Mradi huo ambao umegawanyika katika awamu tatu umekuwepo Chuoni hapo kwa muda wa miaka 10 mfululizo ambapo awamu ya kwanza wamefanikiwa kuongeza elimu kwa watafiti wa SUA na kufanya mafunzo ya aina mbalimbali.

“Katika awamu ya pili tumetengeneza Mitaala kwa ngazi ya Masters na PhD ambapo tumepata mitaala mitatu ambayo imeshaidhinishwa na kupata ithibati ya Tume ya Vyuo Vikuu Nchini,TCU, na inatekelezwa na ina wanafunzi lakini kwa awamu hii ya tatu ambayo tunaelekea mwisho wa Mradi huu tunaamini uwezo wa SUA ambao umejengwa utakuwa endelevu ili kusaidia tafiti zetu kutoa majawabu kwa changamoto za wananchi”, amesema Prof. Sangeda.

Mradi huo wa Kujenga Uwezo kwa Vyuo Vikuu ambao umefadhiliwa na  Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Denmark (DANIDA) utafikia tamati mwezi Desemba mwaka huu.


Mratibu wa Mradi wa Kujenga Uwezo kwa Vyuo Vikuu BSU  Prof. Antony Sangeda

Picha ya pamoja Watafiti wa SUA na Watafiti kutoka nchini Denmark mara baada ya ufunguzi wa Warsha ya Mafunzo ya siku mbili kwa lengo la kujengeana uwezo wa namna ya kutumia matokeo ya kisayansi katika kushawishi jamii pamoja na watunga sera katika kufanya mabadiliko.







Post a Comment

0 Comments