SUAMEDIA

SUA yauomba Uongozi wa Halmashauri ya Rungwe kuzingatia mapendekezo ongezeko la uzalishaji wa Malisho ya wanyama

Na Gerald Lwomile, Rungwe, Mbeya.

 Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeuomba uongozi wa Halmashauri ya Rungwe mkoani Mbeya kuhakikisha unazingatia mapendekezo yaliyotolewa katika mkutano wa kisera ili kuhakikisha kunakuwa na ongezeko la uzalishaji wa malisho ya wanyama wilayani humo.

Prof Chove akikabidhi nyaraka mbalimbali kwa mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Rungwe Bw. Augustino Lawi

 Ombi hilo limetolewa Novemba 12, 2021 na Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Prof. Bernard Chove ambaye pia ni Rasi wa Ndaki ya Kilimo SUA wakati wa Makabidhiana ya Kituo cha Maarifa Ilenge kilichokuwa chini ya Mradi wa InnovAfrica.

 Akisoma hotuba hiyo Prof. Chove amesema katika mkutano wa kisera uliokutanisha wadau mbalimbali zilibainika changamoto kadhaa zinazokabili uzalishaji wa malisho bora ya mifugo ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa mbegu bora za malisho, uhitaji wa taarifa za ufugaji bora na wafugaji wengi hawajafikiwa na huduma ya uzalishaji wa malisho.

 “Kwanza Serikali kupitia huduma za ugani iongeze uelewa wa wafugaji kuhusu malisho haya kwa kutumia shamba mfano na hivyo kuongeza uhitaji wa malisho hayo……., pia wakulima wa mfano watumike kama huduma za ugani ili kuendeleza uzalishaji wa malisho aina ya Bracharia” alisema Prof. Chove

 Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Rungwe wakati wa kupokea Kituo hicho cha Maarifa Ilenge Afisa Mifugo na Uvuvi wa wilaya hiyo Bw. Agustino Lawi amesema utafiti wa malisho uliofanywa na Mradi wa InnovAfrica chini ya SUA umeleta mafanikio makubwa katika wilaya hiyo ikiwa ni pamoja na uzalishaji wa maziwa kuongezeka lakini pia maziwa yake sasa yana ubora unaokidhi viwango bora vya maziwa

 “Ulishaji wa migomba ambao umezoeleka sana katika maeneo yetu mara nyingi umekuwa na matokeo mabaya, kwani unatoa maziwa mepesi na maziwa mepesi hayakubaliki katika soko, kwa hiyo niombe tuendelee kuzalishaji malisho na tuna nafasi ya kuboresha lishe” amesema Bw. Lawi

 Nao wafugaji na wakulima wa mfano katika mradi huo Bw. Kayusi Msigwa na Bibi Tumaini Sigile wamesema kumekuwa na manufaa makubwa katika kilimo cha malisho aina ya Bracharia pamoja na kuwepo kwa changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na malisho hayo kutofanya vizuri katika kipindi cha kiangazi ambapo hata hivyo walishauriwa kufanya umwagiliaji katika kipindi hicho

 Awali akitoa tathimini ya mradi huo Mkuu wa Mradi huo ambao tayari umekabidhiwa kwa Halmashauri ya Rungwe Prof. Dismas Mwaseba amesema katika utafiti wao wameona malisho aina ya Brachiaria Basilisk ndiyo yamefanya vizuri zaidi katika wilaya ya Rungwe

 Mradi wa InnovAfrica umeendeshwa kwa miaka 3 katika wilaya mbili hapa nchini ambazo ni Lindi na Rungwe na kwa upande wa Rungwe mradi huo uliofadhiliwa na Jumuiya ya Ulaya ulilenga kuhakikisha Usalama wa Chakula kwa kuboresha malisho kwa ngombe wa maziwa na kuanzisha Kituo cha Maarifa cha Kijiji ambacho kinaweza kuwasaidia wakulima na wafugaji kujipatia taarifa mbalimbali  za kitaalamu


 Mwakilishi wa Makamu Mkuu wa Chuo na Rasi wa Ndaki ya Kilimo SUA Prof. Chove katikatii aliyevaa tai akiwa katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali walioshiriki katika makabidhiana hayo kulia kwa Prof, Chove ni Mkuu wa Mradi huo uliomaliza muda wake Prof. Dismas Mwaseba



Post a Comment

0 Comments