SUAMEDIA

Viongozi SUA Waaswa kufuata Sheria na Taratibu


 Na:Tatyana Celestine

 Watumishi wa Umma wakiwemo wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA wametakiwa kujua kwa undani Sheria za Utumishi wa Umma, Sheria na Kanuni za Usimamizi wa Fedha na Mali, Sheria za Kazi, Sheria za Ununuzi wa Umma na Utunzaji wa Nyaraka na Siri za Ofisi.


Makamu wa Mkuu wa  Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Pro. Raphael Chibunda akifungua Mafunzo ya Dhana ya Uadilifu na Nafasi ya Uongozi katika Utendaji  na Ufanisi wa Taasisi za Umma nchini katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Morogoro,leo.


Hayo yamesemwa na Makamu wa Mkuu wa Chuo hicho Prof. Raphael Chibunda leo 21 Octoba, 2020 wakati akifungua mafunzo ya Dhana ya Uadilifu na Nafasi ya Uongozi katika Utendaji na Ufanisi wa Taasisi za Umma Nchini kwa wafanyakazi viongozi wa SUA.

Chibunda amesema kuwa mafunzo hayo ni muhimu yakiwa chachu kwa viongozi mbalimbali wa chuo hicho katika mambo muhimu ikiwemo maadili ya utumishi wa umma ambayo yatamsaidia kiongozi kutambua yeye ni mtu wa kwanza katika kuonesha mfano kwa anaowaongoza.

Aidha amewataka viongozi hao kujitoa kushiriki kikamilifu ili kuweza kupata maarifa ambayo yatawajenga kwa manufaa ya sasa na  baadae kwani mafunzo hayo ni mwanzo wa umahiri katika kazi.

Nae mtoa mada katika mafunzo hayo Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Maadili Kazini kutoka Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Fabian Pokela amewakumbusha viongozi hao kuwa mashirika yote ya Umma nchini yamekasimiwa majukumu ili kufikia malengo ya taasisi zao ikiwemo SUA, hivyo Serikali inategemea kuona matokeo chanya yatokanayo na taasisi hizo katika utendaji kazi 

Aidha Pokela amemtaja Rais wa Awamu ya Tano Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kama mfano kwani alipoingia madarakani na jambo la kwanza kulishughulikia likawa ni uadilifu serikalini hivyo SUA inapaswa kuiga mfano huo ili kuweza kufikia malengo iliyojiwekea.

Amesema kuwa katika kufikia malengo lazima kuwe na vipaumbele ambavyo vinawekwa na taasisi pamoja na taifa kitu ambacho wengi wanasahau na kufanya taasisi nyingi kutofikia malengo waliyojiwekea kwa kukosa uadilifu.

Akizungumzia suala la sheria amesema kuwa viongozi wanatakiwa kufuata sheria na kanuni zilizowekwa ili kuweza kumsaidia kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na kusema kuwa ili viongozi waweze kutambua nafasi zao za uongozi ili kuweza kutatua changamoto zinazojitokeza katika maeneo yao ya kazi.

Mafunzo hayo ya Dhana ya Uadilifu na Nafasi ya Uongozi katika Utendaji  na Ufanisi wa Taasisi za Umma nchini ambayo yameandaliwa na SUA kwa watumishi viongozi wa Taasisi hiyo yameanza leo 21/10/2020 hadi 23/10/2020 na yamejumuisha Marasi wa Ndaki, Amidi wa Shule Kuu na wakurugenzi Taasisi na Vitivo, Naibu Rasi wa Ndaki, Naibu Amidi wa Shule Kuu na Makatibu, Wakuu wa Idara za Taaluma na Utawala  na Wakuu wa Idara. 


Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Maadili Kazini kutoka Ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma Bwana Fabian Pokela akiwasilisha Mada ya Dhana ya Uadilifu na Nafasi ya Uongozi katika Utendaji  na Ufanisi wa Taasisi za Umma nchini kwa Viongozi wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA katika Mafunzo ya siku tatu.
Baadhi ya Viongozi walioudhuri mafunzo ya Dhana ya Uadilifu na Nafasi ya Uongozi katika Utendaji  na Ufanisi wa Taasisi za Umma nchini.

Baadhi ya Viongozi walioudhuri mafunzo ya Dhana ya Uadilifu na Nafasi ya Uongozi katika Utendaji  na Ufanisi wa Taasisi za Umma nchini.



Katika picha ya pamoja Makamu wa Mkuu wa  Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Pro. Raphael Chibunda  (katikati waliokaa chini) pamoja na Viongozi mbalimbali wa Chuo hicho wakati wa Mafunzo ya  Dhana ya Uadilifu na Nafasi ya Uongozi katika Utendaji  na Ufanisi wa Taasisi za Umma nchini.



 

Post a Comment

0 Comments