Na Farida Mkongwe SUA - Morogoro
Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kimesema kinaendelea kushirikiana na Wakulima na Wadau wengine wa kilimo katika kuhakikisha Kilimo Ikolojia kinakuwa endelevu kwa kuwa ni kilimo chenye tija na kinachozingatia utunzaji wa mazingira.
Hayo yamebainishwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo
Utawala na Fedha kutoka SUA Prof. Amandus Muhairwa kwa niaba ya Makamu Mkuu wa
Chuo hicho Prof. Raphael Chibunda wakati akifungua Mdahalo wa Siku ya
Chakula Duniani ambao umefanyika chuoni hapo kwenye Kampasi ya Edward Moringe
mjini Morogoro
Prof. Muhairwa amesema katika kuhakikisha Kilimo
Ikolojia kinakuwa endelevu Chuo kimeanzisha Shahada ya Kilimo cha Ikolojia ili
kuweza kuzalisha wataalam watakaoendeleza kilimo hicho.
Awali akizungumza katika Mdahalo huo
Cecile Frobert kutoka Ubalozi wa Ufaransa amesema Ufaransa na wadau wengine wa
kilimo inaendelea na juhudi za kuendeleza Kilimo Ikolojia ambacho
kinasaidia kukifanya kilimo kuwa endelevu huku akitoa wito wa kuepukana na
kilimo cha mazoea cha kutumia madawa ambacho kina madhara kiafya.
Kwa upande wake Jasmien De Winne kutoka Ubalozi
wa Ubeligiji amesema vipaumbele vya nchi hiyo ni kufanya shughuli endelevu za
kilimo zinazolenga kuboresha maisha ya watu na kuwataka wadau wa Kilimo
kujifunza kuendeleza kilimo ambacho hakitaharibu mazingira na kitakuwa na faida
kwa kizazi cha sasa na kijacho
Akizungumzia mdahalo huo Mratibu wa Kituo cha
Kilimo Ikolojia ambaye pia ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Kujiendeleza
ICE- SUA Prof. Dismas Mwaseba amesema kwa muda sasa Chuo kimekuwa kikifanya
tafiti zinazolenga kumuwezesha mkulima kupata zaidi bila kuharibu
mazingira
Kwa upande wao baadhi ya wakulima walioshiriki
katika Mdahalo huo akiwemo Msakuzi Idd na Bahati Swalehe kutoka kata ya Mbuyuni
kijiji cha Kibwaya kilichopo Morogoro vijijini wamesema tangu walipoanza
kutumia Kilimo Ikolojia wameweza kupunguza gharama za kilimo na hivyo kupata
faida zaidi.
Mdahalo huo wa siku moja ambao umehusisha wadau
kutoka SUA , SAT, RECODA, Wakulima,Wanafunzi pamoja na Wadau wengine wa
Kilimo umebeba kauli mbiu isemayo "Kilimo cha Ikolojia kama njia ya kuelekea Mfumo Endelevu wa Chakula".
0 Comments