SUAMEDIA

Tafiti zinazofanyika nchini zisaidie kutumia rasilimali za ndani ili kuleta maendeleo - Prof. Shemdoe

 

Na.Vedasto George, Morogoro

Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Prof. Riziki Shemdoe amewataka watafiti nchini kufanya tafiti  zitakazosaidia kutumia rasilimali za ndani kwa ajili ya maendeleo  endelevu ya uchumi wa viwanda.



Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Prof. Riziki Shemdoe akizungumza na washiriki wa mdahalo hawako pichani katika ukumbi wa Freedom Square Mazimbu

Akizungumza katika mdahalo wa wazi wa uchambuzi wa matokeo ya tafiti katika utunzi wa sera na mipango ya maendeleo uliyoandaliwa  na Mradi wa Uwezeshaji na Uhishaji wa Matumizi ya Matokeo ya Tafiti  katika Uundaji wa Sera  na Mipango ya Maendeleo nchini  uliopo chini ya  Chuo Kikuu Cha Sokoine Cha Kilimo SUA Prof. Shemdoe amesema  ukuaji wa uchumi unategemea tafiti mbalimbali zinazofanywa na watafiti wa ndani.

Pia Prof. Shemdoe ameongeza kuwa tafiti nyingi zinazofanywa nchini zimekuwa zikiishia kwenye majarida na makabati bila ya kuleta manufaa kama inavyotegemewa.

“Pamoja na serikali kutumia matokeo  ya tafiti kutunga sera na mipango ya maendeleo nchini, bado matokeo ya matumizi ya tafiti hizo siyo wa kuridhisha, matokeo  mengi ya tafiti  na taarifa za kitaalamu zinaishia kwenye majarida na makabati na ofisi tu”. Alisema Prof. Shemdoe.

Aidha Prof. Shemdoe ameongeza kuwa mpango wa maendeleo ya serikali wa miaka mitano kuanzia 2016 mpaka 2021 umejikita katika kuhakikisha kuwa kunakuwa na muunganiko wa uwezo wa ndani wa sayansi, teknolojia na uvumbuzi kupitia uwekezaji katika mtaji wa rasilimali watu, taasisi na kuboresha mifumo ya uvumbuzi nchini.

Ukamilifu na utekelezaji  wa ajenda ya mwaka 2030 hasa katika nchi zinazoendelea unategemea sana uwekezaji katika tafiti za kisayansi, teknolojia, ubunifu na uvumbuzi  kwa kuzingatia mahitaji yetu  kwa uhalisia wake”, alisema Prof.Shemdoe

 

 Mratibu wa Mradi wa kuongeza uwezo wa tafiti kusanisi  matokeo ya tafiti Dr.Faith Mabiki  amesema  lengo la mradi huo ni kuchangia katika juhudi za serikali ili kuongeza uwezo  wa watafiti  kusanisi  matokeo ya  tafiti  ili ziweze kutumika  katika maamuzi mbalimbali ya kisera  kwa maendeleo ya  Taifa.

 

Hata hivyo Dkt. Mabiki amesema mradi huo unatekelezwa kwa ushirikiano wa idara mbili ambazo ni Idara ya Kemia na Fizikia pamoja na Idara ya Sera, Mipango na Menejimenti  ya Ndaki ya Sayansi za Jamii  na Insia

 

Akisoma Hotuba ya Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA, Naibu Makamu mkuu wa chuo hicho upande wa Taaluma Prof. Maulid  Mwatawala amesema Bara la Afrika lipo nyuma katika utoaji wa matokeo ya tafiti licha ya kuwa na idadi kubwa ya watu.

Prof. Mwatawala ameongeza kuwa  taarifa ya Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni  la Umoja wa Mataifa (UNESCO) ya mwaka 2015 inaonesha kuwa bara la Afrika linazalisha asilimia 2.6 ya tafiti duniani huku bara hilo likiwa linachangia asilima 2.9 ya watafiti wote duniani.

“ Takwimu hizi ni wazi kuwa uchangiaji wa tafiti kwa maendeleo ya bara la  Afrika na Tanzania ni mdogo” amesema Prof Mwatawala.
Naibu Makamu mkuu wa chuo hicho upande wa Taaluma Prof. Maulid  Mwatawala akitoa hotuba yake

Mratibu wa Mradi wa kuongeza uwezo wa tafiti kusanisi  matokeo ya tafiti Dr.Faith Mabiki akizungumza katika mdahalo huo


Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara Prof. Riziki Shemdoe katikati aliyevaa miwani akiwa na viongozi kutoka vyuo mbalimbali 

Post a Comment

0 Comments