SUAMEDIA

Wakulima, wajasiriamali kunufaika na teknolojia za SUA kupitia AICAD

 Na: Ayoub Mwigune

Wajasiriamali, wakulima na wafugaji nchini wanatarajiwa kunufaika zaidi na teknolojia, mafunzo na ubunifu unaotokana na tafiti za Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia ushirikiano wake na Taasisi ya Kuwajengea Uwezo Wajasiriamali katika Harakati za Kujiletea Maendeleo (AICAD). Ushirikiano huo unalenga kuongeza tija, thamani ya mazao na kipato cha wananchi.

Hayo yameelezwa na Afisa Programu wa AICAD, Bw. Florence Rugimbana, alipokuwa akizungumza na SUA Media katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere wakati wa Maonesho ya Wakulima, Wafugaji na Wavuvi Kanda ya Mashariki yaliyofanyika mkoani Morogoro.

Bw. Rugimbana amesema AICAD hufanya kazi kwa kushirikiana na SUA, vyuo vikuu na taasisi nyingine za utafiti ili kuwafikishia wajasiriamali, wakulima na wafugaji teknolojia na bunifu zinazotokana na tafiti. Amefafanua kuwa jukumu kuu la taasisi hiyo ni kuwa daraja kati ya wabunifu wa teknolojia na watumiaji wake.

Amesema kupitia ushirikiano huo, AICAD hutoa mafunzo kuhusu matumizi ya teknolojia mbalimbali, hususan katika sekta ya kilimo, ili kuwawezesha wananchi kuongeza uzalishaji, thamani ya mazao na kipato chao.

Aidha, amesema taasisi hiyo hufanya tafiti katika jamii ili kubaini changamoto na fursa zilizopo, kisha hushirikiana na taasisi za utafiti kutafuta teknolojia na suluhisho zinazofaa kwa wakulima, wafugaji na wajasiriamali.

“Tumekuja katika Maonesho haya ya Nanenane kwenye banda la SUA kuwafahamisha wananchi kuhusu AICAD na kuonesha baadhi ya bidhaa zinazozalishwa na wahitimu wa mafunzo yetu, ikiwemo bidhaa za mazao ya kilimo zilizoongezwa thamani pamoja na bidhaa zinazotokana na uboreshaji wa kazi za mikono,” amesema Bw. Rugimbana.

Ameongeza kuwa ushirikiano huo unatoa fursa kwa wananchi kupata maarifa, teknolojia na ujuzi unaoweza kuwasaidia kuboresha shughuli zao za uzalishaji, kuongeza ubora wa bidhaa na kupanua fursa za kiuchumi.

Post a Comment

0 Comments