SUAMEDIA

Usalama waimarishwa katika mabanda ya SUA Maonesho ya Nanenane

 Na: Farida Mkongwe

Hali ya usalama imeimarishwa katika mabanda ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwenye Maonesho ya Nanenane, huku Mrakibu wa Polisi Msaidizi katika Idara ya Usalama, Nicholaus Mwantobe, akisema hatua mbalimbali zimechukuliwa kuhakikisha watumishi, wageni na mali zao zinakuwa salama wakati wote.

Mwantobe, ambaye pia ni Mkuu wa Idara ya Usalama SUA, amesema askari wanaendelea kufuatilia hali ya usalama katika maeneo yote ya maonesho, yakiwemo mabanda, maeneo ya maegesho ya vyombo vya usafiri pamoja na sehemu zinazotumiwa na watumishi na wananchi wanaotembelea maonesho hayo.

Amewataka watumishi na wageni kuendelea kuwa waangalifu na mali zao binafsi, akieleza kuwa pamoja na uwepo wa askari, kila mtu ana wajibu wa kuchukua tahadhari kwa kuwa askari hawezi kuwa karibu na kila mwananchi wakati wote.

Aidha, ametoa onyo kwa mtu yeyote mwenye nia ya kufanya uhalifu katika eneo la maonesho, akisema vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga na vina askari wenye weledi wa kutosha.

Amewahakikishia watumishi na wananchi kuendelea na shughuli zao bila hofu, huku akisisitiza kuwa hatua stahiki zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayejaribu kufanya uhalifu.

Post a Comment

0 Comments