SUAMEDIA

SUA kuanzisha Shahada mpya 32 chini ya Mradi wa HEET

Na: Farida Mkongwe

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Mradi wa HEET kinapanga kuanzisha jumla ya kozi (program) mpya za Shahada 32  ambapo timu ya Wanataaluma 32 ambao watahusika na zoezi la kukusanya maoni kuhusu Mitaala mipya ya kozi hizo imekutana kwa lengo la kujadiliana na kushirikishana ufahamu kuhusu yaliyopo kwenye dodoso litakalotumika katika kukamilisha zoezi hilo.


Akizungumza na SUAMEDIA Agosti 10, 2023 Mwenyekiti wa Kamati ya Uratibu wa Uboreshaji na Ukuzaji wa Mitaala SUA Dkt. Jamal Jumanne amesema Chuo kinatarajia kuanzisha Shahada za Juu 20 na Shahada za Awali 12 katika Kampasi Kuu ya Edward Moringe na Kozi 3 za Astashahada  katika Kampasi ya Mizengo Pinda iliyopo Katavi.

“Kama tunavyofahamu katika zoezi hili kuna mitaala mingine itafutwa, kuna mingine itaunganishwa na kuna mitaala ambayo itapewa brand tofauti lakini pia kuna mitaala mipya ambayo itaanzishwa kwa hiyo zoezi la leo lilikuwa ni maalum kwa ajili ya mitaala ambayo Chuo kimeridhia kuanzisha”, amesema Dkt. Jamal.

Akizungumzia lengo la kuwakutanisha Wanataaluma hao Dkt. Jamal amesema ni kujadili na kuwajengea uelewa kuhusu dodoso litakalotumika katika kukusanya taarifa muhimu ambazo zitakusanywa kwa njia ya Mtandao kupitia Jukwaa (Platform) ya Serikali ya Serikali Mtandao yaani e-Government Authoriy (eGA)  

“Hii timu iliyokuwepo hapa ni timu itakayofanya zoezi ambalo kitalaamu tunaliita Market Survey kwenda kuuliza potential employer na potential applicants yaani wale wanaotarajia kuajiri na wale wanaotarajia kuomba kusoma kozi zetu watoe maoni yao juu ya hizi program ambazo tunazianzisha kwamba ni maarifa na ujuzi (skills) gani yaingizwe na yaboreshwe  kwenye hizi program mpya”, amesema Dkt. Jamal.

Nao baadhi ya Wanataaluma walioshiriki katika mafunzo hayo akiwemo Dkt. Prisila Mkenda Mhadhiri kutoka Idara ya Sayansi ya Viumbe Hai na Dkt. Nichodamus Mwasakilali Mhadhiri Idara ya Taaluma za Lugha wamesema wamenufaika na zoezi hilo la kuwapitisha kwenye dodoso litakalotumika kukusanya taarifa hizo.

“Tumenufaika na zoezi hili la kutujengea uelewa wa dodoso hili la ukusanyaji wa taarifa mbalimbali na mahitaji ya hizi Shahada mpya ambazo tunazianzisha huko sokoni, sasa ili kutambua soko letu ni lipi na waajiri pamoja na wanafunzi wanaotarajia kujiunga wanataka nini, tumeelekezana, tumejadili na kuboresha dodoso hili hivyo naamini kazi itakuwa nzuri”, amesema Dkt. Mwasakilali.





Post a Comment

0 Comments