SUAMEDIA

Jamii itambue wanawake wanaweza kuongoza


Na Josephine Mallango 

Vyombo vya habari vimetakiwa kuendelea kuhamasisha jamii kutambua kwamba wanawake wanaweza kuongoza  kihalali na kuwa viongozi bora wenye uwezo wa kielimu , kifani sambamba na kujenga hoja na siyo kwa kupendelewa.


 
Hayo yamejitokeza katika mafunzo ya wanahabari kutoka vyombo mbalimbali mkoani Morogoro yaliyoandaliwa  na Mtandao wa Jinsia Tanzania  TGNP  wakati wa mjadala  shirikishi  wa wanahabari  na muwezeshaji wa mafunzo  hayo Dkt. Rose Ruben kutoka TGNP .

Dkt. Rose amesema kwa kipindi kirefu jamii inamuweka mwanamke kama mtu wa daraja la pili jambo linalopelekea wanawake wengi kujiona hawana thamani ya kuwa viongozi  na ndio maana wao TGNP wamekuwa wakitoa mafunzo kwa wanawake na waandishi wa habari ili kuweza kuleta hamasa na kuinua sauti za wanawake  katika kupata usawa  wa viongozi kwa jinsia zote. 

Ameongeza kuwa Wanaharakati  wanaamini  katika uwezo  wa  wanawake waliopatiwa mafunzo na kupata elimu itawasaidia  kuwajengea  uwezo  wanawake  hao kwa kuwa  Dhana ya  uongozi  kwanza  inaanza na wanawake wenyewe  kuwajibika  na kuonesha  uwezo wa kuwa viongozi. 

‘’Kuhusiana na dhana nzima ya kuhitaji wanawake wawe viongozi,dhana hiyo  inaanzia kwa wanawake wenyewe kuonesha uwajibikaji kwa mwanamke mwenyewe kujiinua thamani yake ya kuwa na utayari wa kuwa kiongozi ili kupata viongozi wanawake ambao wana uwezo wa kuongoza kwa hoja na siyo kwa upendeleo, wanawake  hatutaki  viongozi wa upendeleo tunataka Taifa liwe na viongozi wa ushindani wa kielimu, kifani au hata kuchaguliwa katika vyama vyao tueleweke vizuri hapo  ‘’, amesema Dkt. Rose.

Dkt. Rose amesema pamoja na hatua ya mafanikio iliyopo ikiwepo kuongeza thamani katika Elimu kwa Serikali kuweka elimu bure kwa wote na watoto wa kike kupewa kipaumbele hata wale waliopata ujauzito baada ya kujifungua kurudi shule lakini bado Zipo mila na desturi  zinazosababisha au kukataa  mwanamke  kugombea  au kuchaguliwa na wanawake wenzie ,wanaume au na jamii yote mila hizo ndizo haswa zinazopaswa kuvunjwa 

‘’ Bado kuna mila  potofu  zinazomkandamiza wanamke na kuona siyo kiongozi halali au hapaswi kuongoza  mila hizo zinapaswa kuvunjwa   kwa kuwa zinampelekea  mwanamke kutojiongeza thamani na kujiona yupo yupo tu , mila hizo  na mifumo  hiyo kandamizi  ivunjwe  ndio jambo lililobaki sasa kwa kuwa kuachwa kwa mifumo hiyo kunasababisha wanamke wenyewe  kujiona hawafahi  au jamii kumuona hafai jambo ambalo siyo  sawa kwa kuwa kila mtu ana uwezo wa kuwa kiongozi  halali ‘’

Wanawake wanapaswa kuwa na uwezo wa kushiriki katika nafasi mbalilmbali za uongozi kuanzia ngazi ya familia  mpaka taifa  kwa  kushindana  au kuchaguliwa kwa vigezo vya pamoja  vinavyohitajika  katika nafasi hiyo ya uongozi  ikiwemo kushindana katika nafasi za kisiasa  na kuchaguliwa kwa kuwa wana uwezo na ziada katika uongozi na kuleta maendeleo .

Wakizungumza katika mafunzo hayo wanahabari  akiwemo mwanahabari  Nguli Ratifa Ganzel  kutoka gazeti la Uhuru amesema tatizo lililopo ni ukosefu wa fedha kwa ajili ya kusambaza elimu nchi nzima  hasa katika maeneo yaliyobaki korofi ya mila potofu na mifumo kandamizi ,Elimu ambayo inatakiwa kufika mpaka vijijini  na kuanzia ngazi ya familia ndio  iwe chanzo  kwa kila mmoja kutambua wanawake wana uwezo sawa katika kuongoza  na kuleta maendeleo  na kwamba suala la uongozi haliangalii  jinsi ya kike au kiume bali linahitaji uwezo wa kujenga hoja jambo ambalo wanawake  na wanaume  wana haki  sawa ya kuchagua au kuchaguliwa na kuongoza .










Post a Comment

0 Comments