SUAMEDIA

Wakulima Kiloka, Wilaya ya Morogoro wameiomba Serikali kuwafanyia Utafiti wa Udongo

Na.Vedasto George.

Wakulima wanaojishughulisha na Kilimo cha Mbogamboga na Matunda wa Kata ya Kiloka, Wilaya ya  Morogoro wameiomba Serikali kuwafanyia Utafiti wa Udongo  kwenye maeneo yao ya kilimo ili waweze  kuzalisha mazao yenye ubora yanayoweza kushindana kwenye Soko la kimataifa.



Wakizungumza na SUAMEDIA wakulima Joseph John, Alima Kasimu na Shirima Amani wamesema  kutokana na adha hiyo wanalazimika kutumia viuwatilifu mbalimbali vya kukuzia licha ya kutumia mbegu  bora zenye uhakika wakutoa mazao ya kutosha.

Aidha wamesema  licha ya kuzalisha mazao mengi lakini changamoto kubwa ambayo inaendelea kutishia mazao yao ni uhaba wa soko  ambapo kwa sasa wanalazimika kusafiri umbali wa kilomita 25  kutoka  kiroka mpaka Morogoro mjini lilipo soko la mazao ya mbogamboga na matunda.

Katika kukabiliana na changamoto hiyo Wadau wa Kilimo nchini wanaendelea kuonyesha jitihada za kuwasaidia wakulima kwa   kuwapa mbegu  bora  za mazao ambazo zinatoa mazao mengi  ikiwemo viuwatilifu ambavyo  vinasaidia kuongeza uzalishaji.

Ebenezer Joseph ambaye ni Afisa Kilimo  kutoka Kampuni  ya  Mbegu Tanzania  SEED COM LTD amesema kwa sasa wao kama kampuni wameamua kujikita katika  utoaji wa mbegu  za mazao ya mbogamboga na matunda  lengo likiwa ni  kuwasaidia wakulima ambao wanafanya kilimo  hicho  cha mboga na matunda.


 


Post a Comment

0 Comments