NA:Winfrida Nicolaus
Idara ya Uhandisi Kilimo Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kupitia Mradi wa YEESI Lab inatoa Mafunzo kwa Vijana kuhusiana na Mfumo wa Akili Bandia ili kumsaidia Mkulima kuweza kugundua kwa haraka tatizo kwenye shamba lake bila kumtumia Afisa Ugani.
| PICHA MAKTABA |
Amebainisha hayo Mkuu wa Mradi wa YEESI Lab na Mhadhiri kutoka
SUA Idara ya Uhandisi Kilimo Dr. Kadeghe Fue wakati akizungumza mubashara
kupitia SUA FM kwenye Maonesho ya 29 ya Wakulima, Wafugaji na Wavuvi Tanzania
katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Mkoani Morogoro.
Amesema YEESI Lab ni Mradi
wa Mafunzo kwa vijana ambao unawawezesha kutengeneza mifumo inayoweza kugundua aina za Mimea, Magugu,
Magonjwa na Wadudu waharibifu kwa kutumia picha za Kamera ya kawaida au Simu
ambayo wameita mfumo wa Akili Bandia.
Dr. Fue amesema Mradi
huo utaunda mifumo katika Utambuzi na Uainishaji wa Magonjwa, Magugu, Wadudu
waharibifu pamoja na makadirio ya Miche iliyoota shambani na Utabiri wa Mavuno
na vyote hivyo vitafanywa kwa kutumia Picha za Kamera ya kawaida au Simu Janja.
“Mradi wa YEESI Lab unalenga zaidi katika
kuongeza uelewa kwa vijana wa Morogoro na Mikoa ya Jirani ili kukabiliana na
matatizo mashambani kwa kutumia Simu Janja au picha za kamera ya kawaida ndio
maana tumeita Mfumo wa Akili Bandia ambapo itamfanya Mkulima aweze kugundua kwa
haraka tatizo kwenye shamba lake bila kumtumia Afisa Ugani”, amesema Dr. Fue
Ameongeza kuwa ukiachana
na Mradi wa YEESI Lab kuna Mradi mwingine wa EPA Lab ambao ni Mradi Mama wenye
lengo la kuvitumia Vifaa vya Kielectoniki kwaajili ya Kilimo Bora na cha
Uhakika ili kuongeza Tija kwenye mazao.
Amesema Mradi huo unafanya
kazi kama Maabara ya kutengenezea vifaa vya Kielectroniki vile vile utaenda
kuwasaidia Wakulima katika shughuli zao za shambani ikiwemo kutambua maeneo
yaliyopata shida kwenye shamba lake kwa kutumia vifaa hivyo vya Kielectroniki.
0 Comments