SUAMEDIA

SUA ifanye Tafiti juu ya suala la Chakula hususani mafuta ili kuja na matokeo yenye tija katika Jamii- Mhe: Jaji Mstaafu Joseph Sinde Warioba

 

Na: Editha Mloli

Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Mhe. Jaji Mkuu Mstaafu Joseph Sinde Warioba amelitaka Baraza jipya la Tathlitha ya 13 la Chuo kufanya Tafiti juu ya suala la Chakula hususani mafuta ili kuja na matokeo yanayoweza kuleta tija katika jamii kwa kuwa chuo hicho kinafanya vizuri katika masuala ya tafiti ndani na nje ya nchi.

Mhe. Jaji Mkuu Mstaafu huyo ametoa agizo hilo leo Agosti 19, 2022 katika Hafla ya kushukuru Baraza la Tathlitha ya 12 liliomaliza muda wake na kuzindua Baraza jipya la Tathlitha ya 13 iliyofanyika katika Ukumbi wa Taasisi ya Elimu ya Kujiendeleza ICE chuoni hapo.

Akizungumzia kuhusu utendaji kazi wa Tathlitha ya 12 ambayo imehudumu kwa muda wa miaka mitatu tangu mwaka 2019 ambapo ndipo ugonjwa wa UVIKO -19 uliingia nchini Mkuu huyo wa Chuo amesema analipongeza bazara hilo kwa kazi kubwa waliyoifanya kwa kuongoza na kusaidia kuendesha vizuri masomo kwa wanafunzi wa chuo hicho.

Jaji Warioba amesema japo kuna changamoto nyingi baraza jipya  linapaswa kusaidia katika kubana matumizi ya fedha zilizopo kwa kujifunza kutumia kile kidogo kilichopo kwa ufanisi mkubwa ili kusonga mbele na kufikia malengo ya chuo.

Awali akizungumza mbele ya Mkuu wa Chuo, Makamu Mkuu wa Chuo cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof. Raphael Chibunda hakusita kutoa pongezi kwa Baraza la Tathlitha ya 12 kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kipindi hicho cha miaka 3 tangu Julai 1, 2019 hadi June 30, 2022.

Prof. Chibunda ametaja baadhi ya mafanikio yaliyopatikana katika Baraza la Tathlitha ya 12 ikiwa ni pamoja na mikutano ya kuidhinishwa kwa muundo mpya wa chuo pamoja na upanuzi wa shughuli za chuo kama kuongeza Kampasi ya mkoani Katavi (Kampasi ya Mizengo Pinda), Tunduru Pamoja na Shamba la mfano la Kampasi ya Edward Moringe.

Prof. Chibunda ameongeza kuwa mafanikio mengine yaliyopatikana katika baraza hilo ni pamoja na chuo kutoa watafiti bora nchini ambapo mara mbili mfululizo Chuo kimetoa Mtafiti namba moja ambaye ni Prof. Ludovic Kazwala.

Hafla hiyo imehudhuriwa na watu mbalimbali akiwemo Mkuu wa Chuo cha SUA, Makamu Wakuu wa Chuo, Wajumbe wa Baraza la Tathlitha ya 12 na 13, Wakuu wa Ndaki mbalimbali, Wakuu wa Idara na Vitengo mbalimbali.


 

 







Post a Comment

0 Comments