SUAMEDIA

Wanafunzi wa shahada za juu SUA wang'ara mkutano wa kimataifa wa kisayansi wa ANH2025

 Na: Calvin Gwabara - Dar es salaam

Wanafunzi watatu wa shahada za juu kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) wameiwakilisha vyema taasisi hiyo katika Mkutano wa Kimataifa wa ANH2025 Academy Week 2025 uliofanyika wiki iliyopita jijini Dar es Salaam.

Mwanafunzi wa shahada ya Uzamivu Bw. Eward Mushi kutoka Idara ya Uchumi wa Kilimo na Biashara SUA akiwasilisha matokeo yake ya utafiti kwenye mkutano huo.
ANH Academy Week ni mkutano wa kimataifa wa utafiti unaoandaliwa kila mwaka na Chuo Kikuu cha London cha Usafi wa Mazingira na Tiba ya Kitropiki (LSHTM) tangu mwaka 2016, na hufanyika kwa mzunguko katika nchi za Asia na Afrika lakini mwaka huu, kwa mara ya kwanza, mkutano huo umefanyika Tanzania kwa ushirikiano na SUA kama mwenyeji mwenza.

Licha ya kuwa mwenyeji mwenza SUA iling’aa kupitia ushiriki hai wanataaluma na  Wanafunzi wake watatu wa shahada za juu ambapo Wanafunzi wawili wa shahada ya uzamivu Bw. Eward Mushi kutoka Idara ya Uchumi wa Kilimo na Biashara na Bi. Victoria Kariathi kutoka Idara ya Lishe ya Binadamu na Sayansi ya Watumiaji waliwafanya wasilisho la pamoja kwenye mkuatano huo (Learning Lab) kwa kushirikiana na watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Tufts, Marekani.

Bw. Mushi pia aliwasilisha utafiti wake kwa njia ya mawasilisho ya mdomo kuhusu "Vichocheo vya Kimazingira vya Kiuchumi vinavyoathiri Matumizi ya Matunda na Mboga katika Maeneo ya Vijijini na Mijini Tanzania," na alishiriki kuendesha tukio maalum (Side Event) kwa kushirikiana na ANH Academy, ambapo alitoa uzoefu wa mbinu bora za kufundisha na kujifunza uhusiano kati ya kilimo, lishe na afya.

Kwa upande mwingine, Bi. Rosemary Tegekanya, mwanafunzi wa shahada ya uzamili katika ubora wa chakula na uhakika wa usalama wake kutoka Idara ya Sayansi ya Chakula na Teknolojia, aliwasilisha matokeo ya utafiti wake kuhusu "Tathmini ya Uelewa na Utendaji wa Wakulima kuhusu Matumizi Salama ya Viwatilifu vya Organophosphate katika Mboga Teuliwa kutoka Ilala, Dar es Salaam."

SUA imewapongeza wanafunzi hao kwa juhudi zao za kushiriki katika mkutano huu maarufu wa kimataifa na kutoa wito kwa wanafunzi wengine kuchangamkia fursa za kitaaluma katika majukwaa ya kimataifa ili kuonyesha kazi zao na kupata uzoefu mpya.

Mkutano wa ANH Academy Week unaendelea kuwa jukwaa muhimu la watafiti, wataalamu, na wadau kujadili changamoto na suluhisho mbalimbali kuhusu kilimo, lishe, na afya duniani.


Mwanafunzi wa shahada ya Uzamivu kutoka SUA, Bi. Victoria Kariathi kutoka Idara ya Lishe ya Binadamu na Sayansi ya Watumiaji akiwasilisha matokeo ya utafiti wake.

Bi. Rosemary Tegekanya, mwanafunzi wa shahada ya uzamili katika ubora wa chakula na uhakika wa usalama wake kutoka Idara ya Sayansi ya Chakula na Teknolojia akijibu maswali baada ya kuwasilisha matokeo ya utafiti wake.









Post a Comment

0 Comments